Kwa Mujibu wa Shirika la Habari la Kimataifa la Ahlul-Bayt (as) –ABNA– Mkuu wa Idara ya Mahakama nchini Iran, Hujjatul-Islam Gholam-Hossein Mohseni Ejei, amesema kuwa maadui wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran wameshindwa kufanikisha malengo yao licha ya kutumia uwezo na nyenzo zao zote dhidi ya taifa hilo.
Kwa mujibu wa taarifa iliyonukuliwa kutoka Shirika la Habari la IRNA na Kituo cha Habari cha Idara ya Mahakama, Mohseni Ejei alieleza wakati wa ziara yake katika moja ya majengo ya mahakama mjini Tehran kwamba maadui walipanga njama tatu kuu za kuidhoofisha Iran, zikiwemo kile alichokiita “vita vya siku 12”, “jaribio la mapinduzi la Januari”, na “vita vya siku 40”.
Alisema kuwa licha ya mipango hiyo, maadui walishindwa kufikia malengo yao kutokana na uimara wa Mfumo wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran na umakini wa wananchi wa Iran.
Mohseni Ejei aliongeza kuwa baadhi ya maafisa na wachambuzi walioko upande wa maadui sasa wanakiri kuwa nafasi na hadhi ya Iran katika medani ya kimataifa imeongezeka zaidi kuliko ilivyokuwa hapo awali. Kwa mujibu wake, baadhi yao hata wanaitambua Iran kuwa miongoni mwa mataifa yenye nguvu zaidi duniani.
Aidha, Mkuu huyo wa Mahakama alisema kuwa maadui walitarajia vita vya hivi karibuni dhidi ya Iran visababishe machafuko ya ndani, njaa na kuwafanya wananchi wengi kuyahama makazi yao. Hata hivyo, alisisitiza kuwa matarajio hayo hayakutimia kutokana na mshikamano wa wananchi na nguvu ya taasisi za taifa la Iran.
Your Comment